Aphelenchoides besseyi
Nyingine
Dalili ya wazi zaidi ya ugonjwa huu ni uwepo wa rangi nyeupe kwenye sentimita 3 hadi 5 zilizopo upande wa juu wa majani, ambayo baadae hugeuka kuwa rangi ya kahawia na kisha kufa. Majani machanga, yanayochipuka mara nyingi hujisokota ama hujikunjakunja kadri yanavyokuwa. Kwa kawaida, dalili hizi huonekana bayana zaidi kuanzia kipindi cha katikati ya msimu wa kuotesha hadi kipindi cha kuchipua kwa nafaka. Mara nyingi, mimea iliyoathirika huwa mifupi zaidi na hukosa rangi nzuri ya kijani kama ilivyo kwenye mpunga wa kawaida. Kadri mmea unavyokomaa, vishada vya nafaka huonekana kuwa vidogo kuliko kawaida, na vingi huwa tupu bila nafaka yoyote, hunyauka, ama huumbika vibaya. Katika hali mbaya zaidi, jani la mwisho hujisokota sana kiasi kwamba kishada cha nafaka hushindwa kuchanua kikamilifu kutoka kwenye shina.
Kutumia bakteria wenye manufaa kwenye udongo kama tiba ya mbegu kunaweza kusaidia kuulinda mmea mchanga kwa kuwapunguzia nematodi eneo la kuishi. Kutumia "mbolea za kijani", kama vile kulima mazao fulani na kisha kuyakata na kuyachanganya na udongo, kunaweza pia kusaidia kupunguza idadi ya nematodi kwa kuchochea udongo mzuri ambao kiasili huishambulia minyoo hii. Aidha, tafiti zimeonyesha kwamba, aina fulani ya kuvu wenye manufaa wanaweza kupunguza viwango vya maambukizi kwa kuwashambulia nematodi waliopo kwenye udongo au kwenye mmea.
Daima zingatia kutumia njia mseto zinazojumuisha mbinu za kinga sambamba na tiba za kiasili. Udhibiti wa kemikali kwa kawaida hujikita kwenye kuzitibu mbegu kabla hazijaoteshwa ili kuuwa nematodi wakati wanapokuwa bado wamelala. Kwa kuwa wadudu hawa huishi ndani kabisa ya mbegu, ama kwa kuwa wadudu hawa hulindwa na misokoto iliyojitokeza kwenye majani wakati wa ukuaji, basi vioevu vinavyopulizwa kwenye majani mara nyingi hushindwa kuleta manufaa yanayohitajika. Kama dawa za tiba zikipulizwa shambani, basi hazina budi kupulizwa mapema kwenye hatua za mwanzo za maisha ya mmea ili kuzuia wadudu hawa kusafiri kwenda kwenye vishada vya nafaka. Wakati unapopuliza dawa za kuuwa wadudu ama kemikali, vaa mavazi ya kujilinda, soma maelekezo yaliyopo kwenye lebo za kemikali, fuata kanuni zilizopo kwenye eneo lako, na zingatia mapendekezo sahihi wakati unapochanganya bidhaa ili kuhakikisha kuwa unakuwa salama na unapata matokeo yanayofaa.
Ugonjwa huu husababishwa na minyoo midogo sana iitwayo nematodi, ambayo kimsingi husafiri na kuishi ndani ya mbegu za mpunga. Nematodi hawa wanaweza kuishi kwa kujikausha na kulala usingizi mzito ndani ya mbegu iliyohifadhiwa, kwa hadi miaka mitatu. Pindi mbegu zinapopandwa na kupata maji, nematodi hawa huamka na kuwa hai. Husafiri kwenye mmea kwa kuogelea kwenye utando mwembamba wa maji uliopo juu ya mmea, hasahasa pindi hewa inapokuwa na unyevunyevu mwingi. Huishi na kula tishu za mimea michanga ambayo bado haijakomaa. Kadri mmea unavyokuwa, nematodi hawa huhama kuelekea kwenye maua yaliyochipuka na kisha hujihifadhi kwenye mbegu mpya zilizochipua, na hivyo kuendeleza mzunguko huu.

This page is powered by millions of live Plantix diagnoses. Explore the live agronomic intelligence behind this page with Plantix Intelligence.