Matunzo
Mmea wa pamba ni kichaka cha familia ya Malvaceae, wenye asili ya kitropiki na ya tropiki ya kati ya mikoa ya Amerika, Australia, Afrika, na India. Huoteshwa sana katika nchi zaidi ya 90 kwa ajili ya nyuzi zake pamoja na mafuta ya zao lake. Wigo mkubwa wa aina mbalimbali za pamba mwitu huweza kupatikana Mexico, Australia, na Afrika.
Udongo
Pamba huweza kukua karibia katika aina zote za udongo, ilmradi tu udongo huo uwe na uwezo wa kupitisha maji kwa urahisi. Hata hivyo, kwa ajili ya kupata mavuno mengi, udongo wa michanga tifutifu wenye mfinyanzi wa kutosha, vitu vya kikaboni, na mkusanyiko wa wastani wa nitrojeni na fosforasi ni bora zaidi. Mteremko mzuri unaweza kuwa na manufaa kwani husaidia kukusanya maji katika mwelekeo uliodhibitiwa. pH ya udongo ya kati ya 5.8 na 8 huhitajika kwa ajili ya ukuaji mzuri wa pamba, huku pH ya 6 hadi 6.5 ikiwa safu bora zaidi.
Hali ya hewa
Mmea wa pamba huhitaji kipindi kirefu kisicho na baridi, joto jingi na jua la kutosha ili kupata ukuaji bora. Hali ya hewa ya joto, unyevunyevu pamoja na mvua ya wastani kuanzia sm 60 hadi sm 120 hupendekezwa. Ni mbegu chache tu za pamba zitaota, ikiwa kama hali ya joto ya udongo itakuwa chini ya 15°C. Wakati wa ukuaji amilifu, halijoto bora ya hewa ni 21-37 °C. Mmea wa pamba kwa wastani unaweza kuishi katika joto la hadi 43°C kwa muda mfupi bila kupata uharibifu mkubwa. Mvua za mara kwa mara katika hatua ya kukomaa (kiangazi) na wakati wa siku za mavuno (vuli) hupunguza mavuno katika kilimo cha pamba.